Jumamosi, 13 Aprili 2026 · Dar es Salaam, Tanzania
|
kijijichetumedia.com
Kijiji cha Habari Media
Kijiji cha Habari Media Simulizi za Mageuzi · SDGs · Tanzania
LEO
Fugakuku Business Solution yafunza wafugaji 2,000+ Tanzania — Soma simulizi yake hapa    •    Fugakuku Business Solution yafunza wafugaji 2,000+ Tanzania — Soma simulizi yake hapa    •   

Alhamisi, 4 Juni 2026

Vaileth Kimbe: Kutoka kuuza maandazi hadi kuwainua wasichana 3,000

Vaileth Kimbe, akiwahudumia kuku wake: PICHA/Kijiji Chetu Media
KATIKA Kijiji cha Ngerewaya, Kata ya Mwangata, Manispaa ya Iringa, kuna simulizi ya mwanamke ambaye amegeuza maumivu ya maisha kuwa daraja la matumaini kwa maelfu ya wasichana.

Huyo ni Vaileth Kimbe (32), mfugaji na mjasiriamali ambaye sasa ameanza safari ya kuwainua kiuchumi wasichana zaidi ya 3,000 kupitia mafunzo ya ufugaji wa kuku na ujasiriamali.

Vaileth, kupitia kampuni yake ya VIO FARM, anatarajia kuanzisha kituo maalumu cha mafunzo kitakachowapa wasichana kutoka mazingira magumu maarifa ya ufugaji wa kuku, elimu ya biashara na mtaji wa kuanzia wa Sh. 500,000 kila mmoja baada ya kukamilisha mafunzo ya mwaka mmoja.

Anasema dhamira hiyo imejengwa na uzoefu wake wa maisha pamoja na msaada alioupata kutoka Shirika la CAMFED kupitia mtandao wa CAMA, ambao ulimwezesha kuendelea na elimu wakati alipokuwa akikabiliwa na changamoto nyingi za kifamilia.

“Nilikulia katika mazingira magumu na wakati mwingine niliona kama ndoto zangu hazingeweza kutimia. Lakini nilijifunza kuwa changamoto si mwisho wa maisha, bali ni mwanzo wa kupambana zaidi,” anasema Vaileth.

Akiwa mwanafunzi wa kidato cha kwanza, alianza kuuza maandazi na bagia, ili kusaidia mahitaji ya familia na kumsaidia mama yake. Juhudi hizo ziliendelea hadi alipopata ufadhili wa CAMFED alipokuwa akisoma Shule ya Sekondari Luhota.

Kupitia ufadhili huo alipata sare za shule, madaftari, vifaa vya kujifunzia na fedha za matumizi, mahitaji muhimu yaliyomwezesha kuendelea na masomo bila kukatisha ndoto zake.

Baada ya kuhitimu elimu yake, Vaileth aliamua kuwekeza katika ufugaji wa kuku. Mwaka 2021 alipata mkopo wa Sh. milioni mbili kutoka CAMFED na kuanzisha mradi wa ufugaji wa kuku wa mayai aina ya Sasso.

Leo hii anafuga zaidi ya kuku 600 na huzalisha wastani wa trei 17 za mayai kwa siku. Mafanikio hayo yaliongezeka mwaka 2025 baada ya kupata mkopo wa Sh. milioni 60 uliomwezesha kujenga banda la kisasa lenye uwezo wa kuhifadhi kuku 3,000.

Kwa Vaileth, mafanikio hayo si kwa ajili yake pekee. Anasema lengo lake kubwa ni kuhakikisha wasichana wengine wanapata fursa aliyoipata ili waweze kujitegemea na kufikia ndoto zao.

“Wasichana wengi wana uwezo mkubwa. Wanachohitaji ni mtu wa kuwaamini, kuwapa maarifa na mtaji wa kuanzia. Ninataka kuona wanasimama kwa miguu yao wenyewe na kubadili maisha yao pamoja na familia zao,” anasema.

Ofisa Mifugo wa Wilaya ya Iringa, Daudi Chilagane, anasema ofisi yake imekuwa ikitoa ushauri wa kitaalamu kwa Vaileth ili kuhakikisha anafanya ufugaji wenye tija na unaokidhi viwango vinavyohitajika.

Kwa upande wake, mama yake Vaileth, Felister Nyalusi, anasema anajivunia mafanikio ya mwanawe ambaye amepitia changamoto nyingi tangu akiwa mtoto.

“Alipambana sana tangu akiwa mdogo. Leo hii si tu kwamba amebadilisha maisha yake, bali ameanza kubadilisha maisha ya wengine. Hilo linanipa furaha kubwa,” anasema.

Katika kipindi ambacho changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana inaendelea kuwa miongoni mwa vikwazo vikubwa vya maendeleo nchini, juhudi za Vaileth zinatajwa kuwa sehemu ya suluhisho kwa kuwapa wasichana ujuzi wa vitendo, mtaji na fursa za kujiajiri.

Kupitia kituo chake cha mafunzo kinachotarajiwa kuanza kutoa huduma, maelfu ya wasichana wanatarajiwa kupata maarifa yatakayowasaidia kujenga maisha bora na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya jamii zao.

Kwa Vaileth Kimbe, safari iliyoanza kwa kuuza maandazi na bagia sasa imekuwa mwanga wa matumaini kwa kizazi kipya cha wasichana wanaotafuta njia ya kujikomboa kiuchumi.

Vailth Kimbe akiwa kwenye banda maalumu la kufugia kuku. PICHA: Kijiji Chetu Media


KUHUSU CAMFED

CAMFED (Campaign for Female Education), ni shirika la kimataifa lisilo la kiserikali na lisilo la kibiashara lililoanzishwa mwaka 1993 kwa lengo la kutokomeza umaskini barani Afrika kupitia elimu ya wasichana na uwezeshaji wa wanawake vijana.

Shirika hili linaamini kuwa elimu ni nyenzo muhimu ya kubadili maisha ya mtu mmoja mmoja, familia na jamii kwa ujumla.

Tangu kuanzishwa kwake, CAMFED imekuwa ikifanya kazi katika nchi mbalimbali za Afrika, ikiwemo Tanzania, Ghana, Malawi, Zambia na Zimbabwe. Kupitia programu zake, shirika hilo hutoa msaada wa kielimu kwa wasichana wanaotoka katika familia zenye kipato cha chini ili waweze kuendelea na masomo bila vikwazo vya kifedha.

Msaada huo unajumuisha ada za shule, sare, vitabu, vifaa vya kujifunzia na mahitaji mengine muhimu ya elimu.

Aidha, CAMFED huendelea kuwasaidia wahitimu kwa kuwapatia mafunzo ya ujasiriamali, uongozi, stadi za maisha na fursa za kupata mitaji kwa ajili ya kuanzisha au kuendeleza biashara.

Moja ya mafanikio makubwa ya CAMFED ni kuanzisha mtandao wa CAMA, unaowakutanisha wanawake vijana waliowahi kufadhiliwa na shirika hilo.

Kupitia mtandao huo, wanachama hupeana uzoefu, ushauri na kusaidiana katika miradi ya maendeleo ya jamii; Vaileth akiwa mfano halisi wa matokeo ya mtandao huu.

Tangu mwaka 2005, CAMFED imewafadhili wanafunzi 1,505,478 kuendelea na elimu ya msingi na sekondari katika shule 757 za serikali.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni