![]() |
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Courage House Dar es Salaam, Suzan Shoo, akisimulia jinsi nyumba hiyo salama inavyowapa matumaini mabinti walionusurika ukatili na usafirishaji haramu wa binadamu.
KUNA watoto ambao wamepitia mateso ambayo hata watu wazima hushindwa kuyasimulia bila kutoa machozi.
Wapo waliobakwa wakiwa na umri wa miaka 10. Wapo
waliolazimishwa kujiuza ili familia ipate chakula. Wapo waliosafirishwa kutoka
vijijini kupelekwa mijini kwa ahadi ya kazi nzuri, lakini wakajikuta kwenye
mikono ya watu waliowageuza bidhaa.
Pamoja na maumivu hayo, kuna mahali panapoitwa Courage
House — nyumba salama inayowarudishia watoto hawa utu na matumaini ya kufikia
ndoto zao.
Katika ofisi ndogo yenye utulivu jijini Dar es Salaam,
Suzan Shoo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Courage House Dar es Salaam, anasimulia kwa
sauti ya utulivu, lakini yenye uzito wa maisha ya mamia ya mabinti waliopita
mikononi mwao.
“Tunapokea mabinti waliopitia ukatili wa kingono na
usafirishaji haramu wa binadamu. Wengine wanakuja wakiwa na majeraha ya mwili,
lakini wengi zaidi wanakuwa na majeraha ya ndani kabisa,” anasema.
Safari ya Courage House ilianzia Marekani. Mwanzilishi
wake, Jane Williamson, alikuwa na moyo wa kuwainua wanawake na kuwasaidia
kufikia ndoto zao. Lakini maisha yake yalibadilika alipoona watoto waliokuwa
wanaokolewa na serikali ya nchi hiyo baada ya kupitia ukatili wakikosa mahali
pa kwenda.
Ndipo wazo la kuanzisha nyumba salama likazaliwa.
Kupitia marafiki waliokuwa wakifika Tanzania mara kwa
mara, ndoto hiyo ilivuka mipaka na kufika Moshi, Kilimanjaro, ambako Courage
House ilianzisha nyumba yake ya kwanza salama kwa mabinti waliookolewa kwenye
mazingira ya ukatili.
Leo hii, Courage House inapokea wasichana walio chini
ya miaka 18 kutoka maeneo mbalimbali nchini. Wengine wanaokotwa mitaani,
wengine wanaokolewa kwenye nyumba za mateso, na wengine huletwa na maafisa
ustawi wa jamii, polisi au asasi washirika.
“Mtoto akifika Courage anapewa kila kitu. Malazi,
mavazi, chakula, matibabu, elimu, ushauri nasaha…tunaanza naye upya.”
“Tunapokea baadhi wakiwa na majeraha, wengine
wamebakwa,” anasema Suzan kwa masikitiko.
Suzan anasema baadhi ya watoto wanaopokelewa wanakuja
wakiwa na watoto au wakiwa wajawazito; huku wakiwa na maumivu makubwa moyoni. Anatoa
mfano kwamba walimpokea mtoto aliyekuwa anabakwa na babu yake na mwingine
amebakwa na baba yake hadi kupata ujauzito na kujifungua.
“Tunapompokea tunampa huduma zote hadi kujifungua na
malezi yake na mtoto; kumsaidia kusoma yeye binafsi na mtoto.
“Kwenye kesi ambayo baba amehusika kumbaka binti ni
ngumu sana kuitatua na kumwambia samehe…akimuangalia mtoto anasema huyu si
ndugu yangu lakini ni mwanangu; tunafanya sana unasihi na maombi kwa sababu
huyu anamaumivu makubwa moyoni,” anasimulia Suzan.
Anasema wengi wanakabiliwa na changamoto siyo ya elimu
au chakula pekee, bali uponyaji wa ndani.
Anasema mbali ya ukatili wa kimwili na kihisia, asilimia
47 ya watoto wanaofikishwa Courage House huwa wamekatisha masomo katikati.
“Wengine wameishia darasa la sita, wengine kidato cha
kwanza au cha pili, na baadhi hawajawahi hata kuingia shule.
“Tunawaanzisha shule upya. Kama alikuwa msingi tunamtafutia
shule ya jirani. Kama hakuwahi kusoma kabisa tunamwingiza MEMKWA na wa
sekondari tunampeleka QT. Lengo ni kuhakikisha mtoto anarudishiwa ndoto yake.”
Suzan anasimulia kuhusu mtoto mmoja mwenye miaka 10
waliompokea baada ya kujiingiza kwenye biashara ya ngono. Walipomhoji, alisema
alianza baada ya kufanyiwa ukatili wa kingono nyumbani kwao.
“Alisema mama yake alikuwa anajua,” Suzan anasema kwa
huzuni.
“Ukishakaa na mtoto kama huyu unamrudishaje kwenye
familia ileile bila kubadilisha mazingira? Tunagundua kwamba wakati mwingine si
mtoto tu anayehitaji kuponywa, hata mzazi anahitaji kubadilika.”
Kwa mujibu wa Courage House, asilimia 40 ya watoto
wanaowapokea wana wazazi hai; tatizo ni kwamba wengi wao hawana ‘wazazi salama.’
“Wote hawana wazazi salama, hao wenye wazazi unakuta
ndio waliochangia ukatili. Wazazi wengine wametengana halafu wenza wanaoona nao
wanachangia kwenye ukatili…inategemea na matukio,” anasema.
Suzan anaongeza: “Wakati mwingine mtoto analazimika
kwenda kujiuza ili familia ipate chakula. Hapo huwezi kutatua tatizo kwa
kumrudisha tu nyumbani.”
Kutokana na hali hiyo, Suzan anasema Courage inatoa
huduma za muda mrefu. Mtoto anaweza kubaki Nyumba Salama hadi afikishe miaka
18, akijengewa uwezo wa kujitegemea kabla ya kurudi kwenye jamii.
Anasema katika kipindi hicho, anakuwa ameelewa na
kuona ubaya wa kurudi alikokuwa.
BAADA YA MIAKA 18
Mbali na nyumba ya watoto walio chini ya miaka 18,
Courage House pia ina Transition House kwa waliovuka umri huo. Huko wanajifunza
maisha ya kujitegemea — kuanzia elimu ya fedha, ujuzi wa kazi, hadi namna ya
kuwa raia wema.
Wapo wanaosomea vyuo vikuu na wengine vyuo vya ufundi
na hivyo wanaondoka Courage wakiwa wametimiza lengo la kupata elimu na ujuzi wa
kuwawezesha kwenye maisha yao.
Suzan anatabasamu anaposimulia mafanikio ya mmoja wa
mabinti hao.
“Tunaye msichana ambaye ndoto yake ilikuwa kuwa afisa
ustawi wa jamii. Alikuja kwetu hajamaliza shule. Leo ameajiriwa Courage Moshi
kama afisa ustawi. Mwingine yupo chuo kikuu anasoma Human Resources.”
Lakini hata baada ya watoto kuhitimu na kuondoka
kwenye nyumba salama, Courage House hawaachi kuwafuatilia. Kupitia programu ya
Baba na Mama Fellowship, vijana wanaomaliza masomo hupatiwa msaada wa kuanza
maisha — godoro, gesi, vyombo na hata kodi ya miezi mitatu.
Siyo hivyo tu, Courage House inaendelea kuwafuatilia
kwa upendo kuwapa malezi ya ziada (mentorship), ili wasimame kikamilifu na
kufikia malengo makubwa ya maisha.
“Tunawauliza, kazi inaendeleaje? Unatunza fedha? Una
mipango gani ya maisha?” anasema Suzan.
“Tunataka wajue kwamba bado wanapendwa.”
Suzan anasema lengo ni kuona mbegu waliyoipanda inazaa
matunda ya mafanikio kwa watoto hao.
“Ni kumwambia kwamba umeshakuwa mtu mzima, kuwa raia
mwema wa Tanzania ni hivi, mienendo hii ni sawa, tunatunza fedha namna hii,
kipato chako ni hiki, tunza kiasi hiki. Je, unaenda kanisani au msikitini?
Jenga imani.”
Kwa wale waliokuja na watoto au ujauzito wanapewa elimu
ya malezi na makuzi ya mtoto.
Suzan anaeleza zaidi kwamba mwaka 2022 walifungua
Courage Cafe Moshi Mjini— mgahawa unaouza kahawa na vyakula mbalimbali huku
ukiwa sehemu ya kutoa elimu kuhusu madhara ya usafirishaji haramu wa binadamu.
Anasema Courage inashirikiana na asasi nyingine za kijamii
pamoja na serikali kutoa elimu hiyo.
“Dhana iliyopo ni kwamba watu wanafikiri usafirishaji
haramu wa binadamu unatokea nje ya nchi, ambayo ni nusu ya ukweli. Unatokea
hata ndani ya jamii yetu,” anafafanua.
Anasema ili kutoa elimu endelevu, imeanzishwa kampeni
ya ‘Siyo ndani ya Nchi Yangu’ inyohimiza jamii kuepukana na usafirishaji haramu.
“Pale Courage Café kila anayenunua kikombe cha kahawa
anachangia kuokoa maisha ya mtoto mmoja anayepitia ukatili,” anasema Suzan.
Leo, zaidi ya watoto 150 tayari wamepita Courage House
na kuanza maisha mapya.
Anatoa wito kwa wazazi kuwa karibu na watoto wao, kufuatilia
mabadiliko ya tabia zao, na kujenga mazingira ya kuaminiana.
“Ukiona mtoto alikuwa mchangamfu ghafla anakuwa mkimya
sana…wakati mwingine hiyo ni sauti ya maumivu,” anasema.
“Na mara nyingi wanaowaumiza watoto siyo watu wa
mbali. Ni watu wa karibu kabisa.”
Anahimiza pia wazazi na walezi kuwa wabunifu kwenye
shughuli za ujasiriamali, akisema hivi sasa kuna mikopo yenye masharti nafuu inayotolewa
na serikali kuwezesha biashara ndogo.
“Zipo shughuli nyingi sana za kujiingizia kipato
halali na kutowaingiza watoto kwenye mateso ya ukatili. Wazazi waifuatilie
waanzishe biashara ndogo kwenye mazingira yao,” anashauri Suzan.
MFAHAMU SUZAN
Ni mke na mama wa watoto wawili mwenye shahada ya Maendeleo
ya Jamii na Uchumi.
“Nilianza Courage mwaka 2016 kule Moshi kama afisa
ustawi wa muda nilikuwa nimeajiriwa sehemu nyingine. Nilifanya kwa
muda…nipoanza kazi walikuwa watoto wanne.
“Baadaye nikaajiriwa full time…nikawa meneja wa Nyumba
Salama Moshi, nikafanya kwa miezi kama nane hivi…ilipofika mwaka 2022 baada ya
shirika kuona uhitaji Dar es Salaam nikahamishiwa hapa kama Ofisa Mtendaji
Mkuu…tuna wafanyakazi 15 wa idara mbalimbali.
“Walimu, walinzi, wapishi, walezi na maofisa ustawi wa
jamii. Tumeshahudumia takribani watoto 45 hapa Dar es Salaam tangu tulipoanza
rasmi 2023. Ofisi ilianza mwaka 2022 lakini husuma ya Nyumba Salama ilianza
mwaka uliofuata.
Suzan ni mwanamke anayethamini maisha ya wengine na ndio maana alikubali kufanyakazi na shirika dogo likiwa na watoto wanne pekee. Moyo wake wa kujitolea umeifanya safari yake ya miaka sita ndani ya Courage House kuwa ya mafanikio kutoka ofisa wa kawaida hadi Mtendaji Mkuu wa Taasisi.
Umejifunza nini? Unataka kuchangia mabadiliko chanya kwenye jamii jamii, tuandikie maoni yako hapa nchi.


Hakuna maoni:
Chapisha Maoni