Jumamosi, 13 Aprili 2026 · Dar es Salaam, Tanzania
|
kijijichetumedia.com
Kijiji cha Habari Media
Kijiji cha Habari Media Simulizi za Mageuzi · SDGs · Tanzania
LEO
Fugakuku Business Solution yafunza wafugaji 2,000+ Tanzania — Soma simulizi yake hapa    •    Fugakuku Business Solution yafunza wafugaji 2,000+ Tanzania — Soma simulizi yake hapa    •   

Jumanne, 9 Juni 2026

Utafiti: Majirani kunyunyiza viuatilifu tofauti kunapunguza usugu wa mbu wa malaria

Mwanasayansi, Deogratius Kavishe

 UTAFITI mpya uliofanyika vijijini nchini Zambia umebaini kuwa kunyunyiza viuatilifu tofauti katika nyumba zinazopakana, kunaweza kusaidia kupunguza kasi ya kuenea kwa usugu wa mbu dhidi ya viuatilifu huku ukiendelea kutoa kinga dhidi ya malaria.

Utafiti huo uliochapishwa Mei 17, 2026 katika jarida la Medical and Veterinary Entomology, ulijaribu mbinu ya kunyunyizia viuatilifu katika kiwango cha kaya inayojulikana kama “micro-mosaic”.

Badala ya kutumia aina moja ya kiuatilifu katika jamii nzima, watafiti walitumia viuatilifu tofauti kwa kupishana katika nyumba jirani. Lengo la mbinu hiyo ni kukabiliana na moja ya changamoto kubwa zinazozikabili programu za kudhibiti malaria kwa sasa—kuongezeka kwa usugu wa mbu dhidi ya viuatilifu vinavyotumika kwa kawaida.

Watafiti waliohusika katika utafiti huo ni Dingani Chinula, Kenzo Mumba, Reuben Zulu, Ketty Ndhlovu, Deogratius Kavishe, Neil Philip Hobbs, Samson Kiware, Thomas Reed, Busiku Hamainza na Gerry F. Killeen. Timu hiyo ilijumuisha wanasayansi kutoka Zambia, Tanzania, Ireland na Uingereza, akiwemo wataalamu kutoka Taasisi ya Afya ya Ifakara (IHI).

Usugu wa viuatilifu ni tishio linaloongezeka

Kwa mujibu wa watafiti, usugu wa mbu kwa viuatilifu ni moja ya vitisho vikubwa vinavyoweza kudhoofisha mafanikio yaliyopatikana katika mapambano dhidi ya malaria barani Afrika.

Wanasema mbu wanapoendelea kukutana mara kwa mara na kiuatilifu kilekile, wale wenye uwezo wa kustahimili kemikali hizo huwa na nafasi kubwa ya kuishi na kurithisha sifa hizo kwa vizazi vijavyo. Hali hiyo husababisha viuatilifu kupoteza ufanisi wake taratibu.

Katika utafiti huo, watafiti walilinganisha mikakati mitatu ya upuliziaji wa ndani ya nyumba (Indoor Residual Spraying – IRS), mbinu inayohusisha kunyunyizia viuatilifu kwenye kuta za ndani za nyumba ambako mbu hupumzika baada ya kunyonya damu.

Mikakati hiyo ilijumuisha matumizi ya DDT pekee, matumizi ya mchanganyiko wa clothianidin na deltamethrin pekee, na mfumo wa “micro-mosaic” uliotumia viuatilifu hivyo viwili kwa kupishana kati ya nyumba jirani.

Utafiti ulifanyikaje?

Utafiti ulifanyika katika Wilaya ya Luangwa, Kusini Mashariki mwa Zambia, ambapo watafiti walifuatilia idadi ya mbu katika kaya 135 zilizogawanywa katika maeneo tisa ya vituo vya afya kwa kipindi cha mwaka mmoja baada ya kampeni ya kawaida ya IRS.

Nyumba hizo ziligawanywa katika makundi matatu ya majaribio. Kundi la kwanza lilinyunyiziwa DDT pekee, kundi la pili lilinyunyiziwa mchanganyiko wa clothianidin na deltamethrin, huku kundi la tatu likitumia mfumo wa “micro-mosaic” ambapo nyumba moja ilinyunyiziwa DDT na nyumba inayofuata ilinyunyiziwa mchanganyiko wa clothianidin na deltamethrin.

Katika kipindi cha utafiti, watafiti walifanya jumla ya usiku 1,620 wa kunasa mbu kwa kutumia mitego maalumu ya kisayansi.

Matokeo yalionyesha nini?

Matokeo yalionyesha kuwa idadi ya mbu wanaosambaza malaria ilikuwa ndogo katika makundi yote matatu ya utafiti.

Watafiti hawakubaini tofauti kubwa katika msongamano wa mbu wala aina za mbu waliokutwa chini ya mikakati yote mitatu ya upuliziaji.

“Matokeo hayo yanaashiria kuwa mbinu ya ‘micro-mosaic’ katika kiwango cha kaya inaweza kutoa kinga dhidi ya mbu wa malaria inayolingana na ile ya mbinu za kawaida za upuliziaji, huku ikitoa fursa ya ziada ya kudhibiti usugu wa viuatilifu,” imeeleza ripoti ya utafiti huo.

Aidha, watafiti walibaini kuwa utekelezaji wa mfumo huo ulikuwa rahisi na unaowezekana katika mazingira ya kawaida ya programu za kudhibiti malaria.

Fursa mpya katika mapambano dhidi ya malaria

Kwa mujibu wa watafiti, kuwakabili mbu na viuatilifu tofauti ndani ya jamii moja kunaweza kupunguza shinikizo la uteuzi wa kiasili linalochochea usugu wa viuatilifu.

“Kwa kuwakabili mbu na viuatilifu tofauti ndani ya jamii moja, mbinu ya ‘micro-mosaic’ inaweza kupunguza shinikizo la uteuzi linalochochea usugu, hivyo kufanya iwe vigumu kwa mbu kuzoea na kuwa sugu kwa bidhaa moja tu,” walisema watafiti.

Hata hivyo, wameonya kuwa tafiti zaidi zinahitajika ili kuthibitisha kama mkakati huo unaweza kupunguza usugu wa viuatilifu kwa muda mrefu.

Iwapo tafiti zijazo zitathibitisha manufaa hayo, mfumo wa “micro-mosaic” unaweza kusaidia kuhifadhi ufanisi wa viuatilifu vilivyopo kwa sasa na kuongeza chaguo jingine muhimu kwa programu za kudhibiti malaria katika kulinda jamii dhidi ya ugonjwa huo.

WANASAYANSI WA TANZANIA

Kavishe ni miongoni mwa wanasayansi wa Tanzania walioshiriki utafiti huo, akiwa ni mwanabiolojia wa molekuli anayefanya kazi katika tafiti za malaria ndani ya Idara ya Afya ya Mazingira na Sayansi za Ikolojia katika IHI.

Amepata mafunzo ya kitaaluma katika biolojia ya molekuli na amekuwa akijishughulisha na tafiti za malaria pamoja na magonjwa mengine yanayoenezwa na wadudu kwa zaidi ya muongo mmoja.

Mbali ya Kavishe, mwanasayansi mwingine ni Dk. Samson Kiware, mwenye Shahada ya Uzamivu (PhD) katika Sayansi za Kompyuta za Kihisabati (Computational Sciences).

Kwa sasa ni Mwanasayansi Mkuu wa Utafiti katika IHI, ambako anaongoza Kitengo cha Takwimu za Juu na Uundaji wa Miundo ya Kihisabati (Advanced Statistics & Mathematical Modelling Unit).

Aidha, ana nafasi za kitaaluma za heshima kama Profesa Msaidizi wa Utafiti katika chuo kikuu cha Marquette na Profesa Mshiriki katika Nelson Mandela African Institution of Science and Technology.

Hapo unapoishi, unaweza kushirikiana na majirani zako kuwadhibiti mbu kwa mtindo huu?

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni