
Nyumba ya Star Homes mkoani Mtwara, iliyosaidia kupunguza malaria kwa watoto. PICHA: Ingvartsen Architects/Julien Lanoo.
Kuboresha mazingira ya makazi kunaweza kuwa silaha muhimu
katika kupunguza magonjwa ya watoto nchini Tanzania, kulingana na matokeo ya
utafiti mkubwa wa kisayansi uliofanyika vijijini na kubaini kuwa nyumba bora
zina mchango mkubwa katika kulinda afya za watoto.
Utafiti huo
uliochapishwa katika jarida la Nature Medicine Aprili 21,2026 ulifuatilia
familia zilizoishi katika nyumba maalumu zinazoitwa “Star Homes” katika Mkoa wa
Mtwara na kulinganisha afya zao na familia zilizoendelea kuishi katika nyumba
za kawaida za vijijini kati ya mwaka 2022 na 2024.
Matokeo yake yanaonesha
kuwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano walioishi katika nyumba zilizoboreshwa
walikuwa na viwango vya chini vya malaria, kuhara pamoja na maambukizi ya njia
ya hewa katika kipindi chote cha miaka mitatu ya utafiti.
Utafiti huo umefanywa
kwa ushirikiano wa taasisi mbalimbali za kimataifa na Tanzania, zikiwamo
Taasisi ya Afya Ifakara (IHI), CSK Research Solutions, University of Oxford,
Royal Danish Academy, Durham University, Amsterdam UMC pamoja na Mahidol-Oxford
Tropical Medicine Research Unit.
Watafiti kutoka
Ifakara waliohusika ni pamoja na Arnold Mmbando na Ally Olotu.
Katika utekelezaji wa
mradi huo, nyumba 110 za ‘Star Homes’ zimejengwa katika vijiji 70 nchini mwaka
2021 na familia zilihamia kati ya Juni na Desemba mwaka huo.
Kuanzia Januari 2022,
watoto 247 walioishi katika nyumba hizo walifuatiliwa pamoja na watoto 936
waliokuwa wanaishi katika nyumba za kawaida.
Ufuatiliaji wa afya
ulifanywa kwa miaka mitatu kupitia ziara za kila wiki zilizofanywa na watafiti.
Matokeo yalionesha
kwamba asilimia 98 ya watoto katika makundi yote mawili walikuwa wakitumia vyandarua,
jambo lililowasaidia watafiti kubaini kuwa tofauti za kiafya zilichangiwa zaidi
na mazingira ya makazi kuliko matumizi ya vyandarua pekee.
NYUMBA NI SEHEMU
YA KINGA YA MAGONJWA
Matokeo hayo yanakuja
wakati nchi nyingi za Afrika zinakabiliwa na changamoto zinazoongezeka za
mabadiliko ya tabianchi, usugu wa dawa na viuadudu vinavyotumika dhidi ya mbu,
pamoja na mifumo ya afya yenye mzigo mkubwa wa wagonjwa.
Moja ya ujumbe mkubwa
wa utafiti huo ni kwamba mapambano dhidi ya magonjwa hayawezi kutegemea
hospitali na dawa pekee, bali yanahitaji pia mazingira bora ya makazi.
“Uboreshaji mkubwa wa
usanifu wa nyumba za vijijini una uwezo wa kuleta athari kubwa ya kiafya katika
maeneo ya Afrika yenye joto na unyevunyevu,” watafiti wamefafanua.
Kwa mujibu wa matokeo
hayo, asilimia 44 ya watoto walioishi ‘Star Homes’ walikuwa na maambukizi
machache ya malaria, wakati magonjwa ya kuharisha yalipungua kwa asilimia 30 na
ni asilimia 18 pekee waliokuwa na maambukizi ya njia ya hewa; ikilinganishwa na
watoto walioishi katika nyumba za kawaida za vijijini.
Utafiti huo pia
ulionesha maboresho katika ukuaji wa watoto pamoja na kupungua kwa tatizo la
udumavu.
“Maambukizi ya
magonjwa haya matatu makubwa yanayosababisha vifo vya watoto yanahusishwa kwa
karibu na mazingira ya nyumbani,” wanaeleza watafiti.
UPEKEE WA STAR
HOMES
Star Homes zilibuniwa
mahsusi kupunguza hatari za maambukizi kupitia mifumo mbalimbali ya kisasa ya
mazingira na afya.

Mwonekano wa nyumba bora za vijijini Mtwara/PICHA: Ingvartsen Architects/Julien Lanoo.
Sifa ya kipekee ya nyumba
hizo ni kwamba zina madirisha yenye nyavu za kuzuia mbu, mfumo bora wa kuingiza
na kutoa hewa, maeneo safi ya kupikia, mifumo ya kuvuna maji ya mvua, nishati
ya jua, vyoo bora vya usafi wa mazingira na milango inayojifunga yenyewe kuzuia
wadudu kuingia.
Nyumba hizo
zinazojengwa kama ghorofa, vyumba vya kulala viliwekwa katika ghorofa ya juu,
ili kupunguza uwezekano wa kung’atwa na mbu ambao mara nyingi huruka karibu na
ardhi.
Zimetengenezwa kwa
kutumia mbinu zinazotegemea mazingira ya asili bila matumizi makubwa ya
nishati.
Watafiti wanasema
nyumba nyingi za kawaida vijijini huwaweka watoto katika hatari kubwa kutokana
na kung’atwa na mbu, kuvuta moshi wa ndani, hewa duni, uhifadhi usio salama wa
maji na msongamano wa watu.
Kwa mujibu wa
utafiti, changamoto hizo zinatatuliwa kwa wakati mmoja na ‘Star Homes’ na hivyo
kutengeneza mazingira salama zaidi kwa watoto na familia zao.
“Nyumba bora zinaweza
kupunguza mzigo wa magonjwa matatu hatari kwa watoto na kuboresha ukuaji wao,”
watafiti wanafafanua.
STAR HOMES
Ni nyumba zilizobuniwa
na kampuni ya Ingvartsen Architects chini ya uongozi wa Jakob Knudsen.
Kwa mujibu wa
uchambuzi wa awali wa kiuchumi, nyumba hizo; zinatumia saruji kwa kiwango cha
chini kwa asilimia 73, zinapunguza uzalishaji wa hewa ya ukaa kwa asilimia 57 na
zilikuwa nafuu kwa asilimia 24 ukilinganishwa na nyumba za kawaida za saruji
vijijini
Watafiti wanaamini
matokeo hayo yanaweza kuwa muhimu kwa mustakabali wa Afrika, hasa wakati ambapo
idadi ya watu barani humo inatarajiwa kuongezeka kutoka bilioni 1.5 hadi zaidi
ya bilioni 3.7 ifikapo mwaka 2070.
Katika mazingira
hayo, mahitaji ya mamilioni ya nyumba mpya yataongezeka, na tafiti kama hizi
zinaonyesha kuwa nyumba hizo zinaweza kujengwa kwa njia ambayo si tu inalinda
mazingira, bali pia inalinda afya za watoto.
MUUNDO WA UTAFITI
NA WASHIRIKI
Ulikuwa ni utafiti wa
majaribio uliokuwa wazi kwa washiriki na watafiti (open-label), uliotumia mfumo
wa makundi ya kaya (household-cluster) pamoja na upangaji wa nasibu wenye
udhibiti (randomized controlled trial), ambapo kila kijiji kilitumika kama kitalu
cha utafiti. Utafiti huo ulifanyika kuanzia Januari 2022 hadi Desemba 2024.
Utafiti huo ulifanyika
katika maeneo ya vijijini ya Mkoa wa Mtwara nchini Tanzania, karibu na mpaka wa
Msumbuji.
Mkoa huo ulichaguliwa
kwa kuwa ulikuwa miongoni mwa mikoa yenye kiwango kikubwa zaidi cha maambukizi
ya malaria nchini mwaka 2023, ikiwa katika nafasi ya pili kitaifa. Aidha, kwa
ujumla, asilimia 67.3 ya wakazi wa Mtwara walikuwa na upatikanaji wa vyandarua
vyenye dawa ya kuua wadudu (ITNs).
Watafiti walifanya
uchunguzi katika kaya 14,600 zilizopo katika vijiji 70 ambapo zilipatikana 862
zilizokuwa na sifa ya kushiriki.
Vigezo vilikuwa kukubali kushiriki katika utafiti kwa hiari, ikiwemo ufuatiliaji wa afya kwa kipindi cha miaka mitatu; kumiliki eneo la kutosha kujenga nyumba mpya; kaya kuwa na watoto watatu wenye umri chini ya miaka 13; na kuishi katika nyumba yenye kuta za udongo, paa la nyasi na sakafu ya udongo, ikiwa na choo cha shimo, bila umeme wala maji ya bomba.
Je, nyumba bora zinaweza kuwa silaha mpya ya kupambana na magonjwa ya watoto Tanzania?

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni