![]() |
| PICHA: RESTUTA JAMES |
Ule msemo wa anzia ulipo ukiwa na ndoto kubwa,
umetafsiriwa kwa vitendo na nembo ya Bella Ragazza,
iliyoasisiwa na mwanadada, Anna Ambroce, aliyeanza kutengeneza vikapu asilia
akiwa na mwanamke mmoja mfumaji.
Safari ya Bella Ragazza ilianza mwaka 2018, lakini
miaka saba baadaye, tayari alikuwa na wanawake 200 wanaofanyakazi hiyo na
kujiingizia kipato cha uhakika.
“Tulianza tulikuwa na mama mmoja mwaka 2018, sasa hivi
tuna wamama 200, ambao 100 wapo mkoa wa Iringa na 100 wapo Njombe,” anasema
Shani ambaye ni meneja katika kampuni ya Bella Ragazza.
Aidha, anasema kazi hiyo imewezesha wanawake na vijana
katika mikoa hiyo kujikwamua kiuchumi na kufungua biashara nyingine katika
maeneo yao, baada ya kupata mitaji.
![]() |
| PICHA: RESTUTA JAMES |
“Wengi tofauti na maisha waliyokuwa wanaishi, maisha
yameboreka. Wamejenga wengine wamefungulia biashara wanaume wao...kuna kijana ana
miaka 21 amefungua saluni, amejenga, amenunua bodaboda na anamsaidia mama yake,”
anaeleza.
Aidha, anasema pamoja na mafanikio hayo, wanakijiji
hao wanakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa majani, kwani wafugaji
wanayatumia kwa malisho na kisha huyachoma moto baada ya kuchunga ng’ombe.
“Changamoto kubwa ni majani mwanzoni walikuwa
hawanunui, lakini sasa hivi wananunua...kule Iringa wafugaji wanaingiza sana
ng'ombe porini halafu wakishalisha ng’ombe, wanachoma moto, kwa hiyo
hawawaruhusu wale wamama kuchukua yale majani. Inawalazimu wale wamama waende
Singida kununua,” anafafanua.
Shani anasema umbali wa kufuata majani unaongeza sio
tu gharama ya usafiri bali pia usumbufu wa kulipa ushuru njiani.
“Wasipokuwa na kibali cha maliasili ni lazima ulipe
ushuru, kwa hiyo inawawia vigumu sana kushona vikapu, sio kama ilivyokuwa
mwanzo.
“Sasa hivi unaweza kuwaambia wakufumie vikapu 1,000
huwezi kupata vyote, utapata 500, kwetu ni changamoto kwa sababu unakuta kuna mtu
wa jumla anavitaka. Je, utampa mtu wa jumla halafu dukani ukaacha usiweke.
Inakuwa changamoto,” anasema Shani.
Anasema kikapu nacho kinalipiwa ushuru wa Sh. 500 hali
ambayo inawakatisha tamaa baadhi ya wanawake ambao wangetamani kufuma vikapu
katika muda wao wa ziada.
![]() |
| PICHA: RESTUTA JAMES |
“Alipe ushuru, kibali, asomeshe watoto, alishe
familia...hiyo hiyo hela ya vikapu. Ni changamoto.
“Ushauri wangu kwa serikali ni kwamba ipunguze ushuru
na wale walioko kwenye halmashauri wangetembelea kwanza hivi vijiji. Mfano...Iringa
wanaoshona vikapu wananyanyaswa sana na wafugaji...wanapeleka ng’ombe kula yale
majani, wakimaliza kulisha wanachoma moto. Kwa hiyo hawa watu wa halmashauri
wangewatembelea wajasiriamali wadogo kama hawa kujua changamoto zao...sio kukaa
tu ofisini unaletewa makusanyo ya ushuru.
“Kwa kweli Halmashauri ndizo zinazotudidimiza,”
anasema.
Anaongeza kuwa ili kukabiliana na changamoto hiyo, Bella
Ragazza, imelazimika kukata kibali cha mwaka na kuwapatia wanawake wanaofanya
nao kazi, ili kuwapunguzia usumbufu na kuwarahisishia kazi.
“Wamama hawana uwezo wa kulipa hizi gharama na zaidi
sana watakata tamaa kwa hiyo sisi tuliamua kubeba hizi gharama,” anafafanua
Shani.
MAFANIKIO
Pamoja na changamoto hizo, Bella Ragazza, inauza
vikapu hivyo sio Tanzania pekee bali nje ya nchi hasa Ulaya na Marekani.
Bella Ragazza ni neno la Kiitaliano linalomaanisha
“mwanamke mrembo,” lilichaguliwa na Anna baada ya kukaa kwa muda na Waitaliano
na kuvutiwa na lafudhi yao.
Anna mzaliwa Iringa ambaye alibaini fursa ya soko la vikapu
vya ambavyo alianza kwa kununua 53 kwa lengo la kuviongezea thamani.
Alianza na mtaji wa Sh. 500,000 akiwa peke yake, hivi
sasa imeajiri watu kadhaa na kuwezesha wanawake na vijana 200 ambao wamepata
soko la uhakika la vikapu, mikeka na viatu vya ngozi.
Nembo ya Bella Ragazza hutengeneza bidhaa zake kwa
mikono, jambo linalofanya kila kipande kuwa cha kipekee na vya kuvutia sana.





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni