Jumamosi, 13 Aprili 2026 · Dar es Salaam, Tanzania
kijijichetumedia.com
Kijiji cha Habari Media
Kijiji cha Habari Media Simulizi za Mageuzi · SDGs · Tanzania
LEO
Fugakuku Business Solution yafunza wafugaji 2,000+ Tanzania — Soma simulizi yake hapa    •    Fugakuku Business Solution yafunza wafugaji 2,000+ Tanzania — Soma simulizi yake hapa    •   

Jumatano, 25 Machi 2026

Miaka miwili ya kushindwa ilivyobeba mafanikio kwenye ufugaji wa kuku

Christowelu akiandaa vifaranga


Habari mbaya za kutofanikiwa kwa kilimo cha matikiti miaka ya 2014 pamoja na ufugaji wa samaki kutofanya vizuri sokoni, hazikufanikiwa kuua ndoto ya Dk. Christowelu Zephania.

Badala yake, habari hizo zilimfanya atafakari kwa kina kile alichopenda kukifanya kutimiza lengo lake la kuipa jamii suluhisho la uhakika katika ufugaji; ndipo wazo la Fuga Kuku Business Solution, likazaliwa na kuanza kuchanua rasmi.

Christowelu, Mkurugenzi na Mwanzilishi wa kampuni ya Fugakuku Business Solution, ambaye kitaaluma ni daktari wa mifugo, amefanikiwa kubadilisha ndoto za wafugaji zaidi ya 2,000 kuwa miradi ya kibiashara.

Anasema alipohitimu chuo cha mifugo Buhari kilichopo mkoani Tanga, alipata ajira ambayo aliitumikia kwa wiki moja pekee na kuamua kujiajiri kwa lengo la kuwa miongoni mwa watu wanaoleta masuluhisho kwenye changamoto zinazoikabili jamii.

Anasema alilazimika kufanya hivyo akiuza utaalamu wake kwa kuwafundisha wafugaji wapya ambao hawajui chochote kuhusu ufugaji wa kuku, mbinu za ufugaji wa kibiashara, aina za kuku, dawa, chakula, usafi na uzingatiaji wa chanjo.

Mwanadada Christowelu, anasema kuku wanaofaa kufugwa kibiashara ni wa nyama, mayai na chotora; akishauri kwamba kwa mfugaji mdogo anashauri aanze kufuga kuku wa nyama ambao wanaweza kurudisha uwekezaji na faida baada ya siku 28.

Anasema safari yake ya ujasiriamali ilianza mwaka 2014, kwa kushirikiana na mume wake, walikuwa wanafanya miradi mitatu ya ufugaji wa kuku, samaki na kilimo cha matikiti; miradi ambayo haikuwapa matokeo waliyoyakusudia.

Anasema wakulima wao walishindwa kushindana sokoni hususani wa samaki ambao mazao yao hayakuwa na samaki wakubwa kama ilivyotarajiwa.

“Tulifanya samaki, watu hawakupata matokeo mazuri, kwa sababu samaki kwenye soko liliwashinda…mtu anategemea kupata samaki wakubwa, anapata wadogo wadogo kwa hiyo mfugaji anaingiza pesa lakini hapati faida…na kwenye matikiti vile vile…ndipo tukafikiria tufanyeje…tukajikita kwenye ufugaji kuku.

“Mwaka 2016…ndio tukajikita sasa, tukaangalia ni kitu gani ambacho mfugaji yeyote anaweza kufanya kwa urahisi na kikamletea matokeo. Tukaamua kubaki na mradi mmoja wa kuku peke yake.

“Tunawafundisha namna ya kulea vifaranga, makundi ya chakula, dawa na kubwa zaidi usafi wa vyombo vya chakula…aina zote tatu za kuku zinamakundi tofauti ya vyakula.

“Kwenye ufugaji wa kuku kuna changamoto mbili…mtaji na magonjwa ya kuku. Watu wengi wanaanzisha miradi ya kuku wanaishia katikati kwa sababu ya kuingiliwa na magonjwa. Namna ya kukabili magonjwa ni kwa kuzingatia chanjo, lakini kubwa ni bio security (usafi), kuzingatia usafi kwenye mabanda, vyombo vya chakula na mazingira yote kwa ujumla,” anasema.

Christowelu akiwa kwenye moja ya mradi wa kuku


Christowelu anasema kwenye ufugaji wa kuku kibiashara, wameona matokeo makubwa na wateja wao wanapata matokeo waliyoyakusudia.

“Kwa hiki ninachofanya, naona wafugaji wakifanikiwa…kuku ni pesa, kuku ni biashara rahisi kukua,” anasema.

Christowelu anasema Fugakuku ni biashara ya familia, akishirikiana na mume wake ambaye ni mtaalamu wa majengo (architecture).

“Kwenye ujenzi wa mabanda yeye ndilo eneo lake hasa. Tukija kwenye menejimenti na ufugaji kibiashara mimi ndio naingia. Yeye pia anajua kila kitu kuhusu kuku,” anasema.

Christowelu ambaye ametoa mafunzo kwa zaidi ya wafugaji 2,000, anasema changamoto anayoiona kwa jamii ni kutokuwa na taarifa kuhusu ufugaji.

“Watu wengi bado hawana taarifa za kuku…tumefanya hii kazi kwa miaka 10 sasa, watu wanamchukulia kuku kama ni ndege mdogo, ambaye hana thamani. Unaweza ukamtembelea mfugaji akadhani kujenga banda la kuku 2,000 ni Sh. 300,000…changamoto nyingine ni mitaji. Ili uweze kufanya kwa ukubwa lazima uwekeze kikubwa. Kuku huwezi kufanya kwa Sh. 100,000,” anafafanua.

Kuhusu mtaji alioanza nao yeye, Christowelu anasema walikopeshwa kiasi cha fedha na wazazi wa mume wake, ambacho walitumia kununua vifaranga na kulipa fedha kidogo kwa ajili ya mashine ya kutotolesha vifaranga.

“Lakini pia tulikuwa tunauza utaalamu kwa maana ya kufundisha watu, tunatembelea mashamba ya wafugaji na tuliendelea kutumia mitandao ya kijamii kujitangaza.

“Tumehudumia zaidi ya watu 2,000…tumeanyakazi Dodoma, Morogoro, Geita, Arusha, Mbeya, Tanga na Mtwara na hapa Dar es Salaam ambako ndipo zilipo ofisi zetu. Mikoa mingine tumeuza ujuzi, vifaa na vifaranga.

Kwenye ujuzi anasema Fugakuku Business Solution, inatoa elimu kuhusu ufugaji wa kuku, makundi ya chakula, muda wa kuwalisha, utoaji wa chanjo na usafi wa mabanda na vyombo vya chakula.



Anasema wanauza pia vifaranga, wanajenga mabanda na wanasambaza vifaa vya kuku kama incubator.

“Kuku ni pesa inayotembea…ninatoa rai kwamba watu waanzishe mradi wa kuku. Anza tu ukiwa mdogo, chini kabisa anza na kuku 200. Unaweza kuongeza kuku hadi mara tatu kwa mwaka. Ni mradi ambao unakufanya uendelee na shughuli zako kama kawaida, zingatia usafi na chanjo,” anasema.

Kuhusu matumizi ya mitandao anasema ndiyo iliyobadilisha maisha yao kwa kuwa ni jukwaa linalowapatia wateja ndani na nje ya Dar es Salaam.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni