Kwa kifaa kidogo
kinachobebwa mkononi, wahudumu wa afya wanaweza kujua kwa wakati halisi kama
mgonjwa amemeza dawa—au ameacha.
Ubunifu huu wa
kidijitali kutoka Taasisi ya Afya Ifakara (IHI), unalenga kupunguza usugu wa
dawa na kuboresha matokeo ya matibabu.
Kwa lugha rahisi ni
kwamba Wise
Pill Box ni kisanduku janja cha dawa kinachozungumza na hospitali.
Kila mgonjwa anapokifungua
kuchukua dawa taarifa hutumwa moja kwa moja hospitalini, mfumo huandika muda
halisi wa matumizi ya dawa na kama hakijafunguliwa, tahadhari hutumwa.
Mtafiti Mkuu wa
miradi ya TB katika Taasisi ya Afya Ifakara (IHI), Dk. Beno Mbeya, anasema kifaa
hicho kinamsaidia mtoa huduma za afya kufuatilia wagonjwa wake wa TB kwa
urahisi na kutoa ushauri kwa wakati.
Anasema kifaa hicho
kinampa taarifa mtoa huduma wa afya aliye hospitali pale mgonjwa anapomeza dawa
au asipomeza; kikirekodi muda aliomeza.
“Ni kifaa
kinachochajiwa na kinakaa na chaji kwa miezi mitatu…mgonjwa akikifungua kinatoa
taarifa hospitali kwenye simu au kompyuta. Mgonjwa asipomeza dawa pia kinatoa
taarifa. Inakuwa rahisi mtoa huduma kumfuatilia mgonjwa na wakati mwingine
unaweza kumpigia simu kumkubusha kumeza dawa,” anasema.
Anakumbusha kwamba matibabu
ya TB kwa kawaida huwa ni ya muda mrefu; ikiwa ni miezi sita kwa wagonjwa wa
kawaida na inafika miezi tisa mpaka 24 kwa wale ambao wana kifua kikuu sugu.
“Kutumia dawa za
kifua kikuu huwa zinakuwa nyingi, unaweza kupewa dawa tofauti tofauti nne, na
unameza kwa miezi sita kila siku bila kusimama. Usipomeza kama inavyotakiwa unatengeneza
usugu, unaweza usipone, unaweza ukasambaza wadudu zaidi…na tunajua kuna athari
za hizi dawa za TB, kwa hiyo ili kuhakikisha mgonjwa anameza hizi dawa, kwa
wakati, kila siku bila kupoteza dozi, tunatumia digital technology,
kuhakikisha kwamba kweli mgonjwa anameza dawa.
“Tunaweka dawa kwenye
wise pill box, anaenda nacho nyumbani, ule muda wa kunywa dawa ukifika,
akikifungua, sisi tunapata ujumbe.
“Inatuambia mgonjwa
amemeza dawa saa ngapi na kama hajafungua, tunajua mgonjwa huyu hajameza dawa;
hii ndio device ambayo tunaitumia.
“Tumeanza kukitumia
mwaka juzi (2024), lakini bado kipo kwenye majaribio, ila kinaleta matokeo yenye
matumaini.
“Utafiti huu kwa sasa
tunaufanyia Hospitali ya Rufaa Mwananyamala, sisi Ifakara tuna kituo chetu cha
utafiti ambacho tunafanya tafiti za kifua kikuu.
Huu mradi una awamu
tofauti tofauti, awamu ya kwanza ilikuwa na wagonjwa 28 na hao walipewa hii device,”
anafafanua Dk. Mbeya.
Naye Mfamasia Mtafiti wa dawa na chanjo katika taasisi hiyo, Beatus Simon, anasema mgonjwa anapokuwa amemeza dawa, taarifa inayopokelewa inaonesha muda na kuweka alama ya bluu wakati kwa wale wasiomeza dawa inatuma taarifa ya kijivu.
Anasema mgonjwa wa TB anapaswa kuzingatia umezaji wa dawa katika muda unaofanana kila siku, ili kuhakikisha vimelea havipati usugu wa dawa.
Wakati wakibaini
kifaa hicho, takwimu zinaonesha kwamba Mkoa wa Dar es Salaam (Temeke), unaongoza
kwa ugonjwa wa TB; ikifuatiwa na Kilimanjaro, Dodoma, Mbeya na Mwanza.
Aidha, Tanzania ni
miongoni mwa nchi 30 zenye mzigo mkubwa wa TB unaotajwa kuwa miongoni mwa
magonjwa hatari zaidi ya kuambukiza duniani licha ya uwepo wa matibabu.
Hata hivyo, hapa
nchini visa vipya vimepungua kwa asilimia 44, kutoka wagonjwa 306 kwa kila watu
100,000 mwaka 2015 hadi 172 kwa kila watu 100,000 mwaka 2024.
Taarifa ya Shirika la Afya Duniani (WHO) ya Mwaka 2024, inaonesha kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika kupunguza maambukizi mapya ya ugonjwa huo.
Aidha, vifo vitokanavyo na ugonjwa vimepungua kutoka 56,000 mwaka 2015 hadi vifo 23,500 mwaka 2024, sawa na punguzo la asilimia 59. Kiwango hiki kimepelekea Tanzania kuwa miongoni mwa nchi chache duniani zilizo katika hatua nzuri ya kufikia lengo la dunia la kutokomeza ugonjwa huu ifikapo 2030.
MWANASAYANSI
NYUMA YA UVUMBUZI
Nyuma ya mafanikio
haya yupo Dk. Beno Mbeya, ambaye ni daktari bingwa wa magonjwa ya mapafu, akiwa
ameongoza tafiti kadhaa za TB (Optirimox, STEP 2C, DECODE TB).
Ana utaalamu katika
afya ya umma na teknolojia za afya, kazi yake inaunganisha sayansi, teknolojia
na maisha halisi ya wagonjwa.
Mwanasayansi huyo ambaye
ni mtafiti katika Taasisi ya Ifakara (IHI), tangu mwaka 2013.
Ana msingi imara wa
kitaaluma na uzoefu mpana wa kitaalamu katika nyanja ya afya ya umma. Ana shahada
ya Udaktari wa Tiba (Doctor of Medicine) kutoka Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi
Shirikishi Muhimbili, Shahada ya Uzamili ya Sayansi katika Afya ya Umma (MSc
Public Health), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na kabla ya hapo, alipata
pia Shahada ya Uzamili ya Utawala wa Biashara (MBA) kutoka chuo hicho.
Dk. Beno kwa sasa
anasoma Shahada ya Uzamivu (PhD) katika Afya ya Umma katika Chuo Kikuu cha
Nicaragua (Hispania), ambapo anatarajiwa kuhitimu mwaka huu 2026.
Mbali na hilo, Beno
anatoa huduma zake kama Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Mapafu (Consultant
Pulmonologist); anashirikiana na taasisi na mashirika mashuhuri kama Medical
Association of Tanzania, mtandao wa TB Net consortium, pamoja na vikundi
mbalimbali kama Trial Methodology Research Partnership (TMRP)/NIHR nchini
Uingereza. Mchango wake unahusisha maeneo mbalimbali ikiwemo tathmini ya
matokeo ya tiba, mifumo ya taarifa za afya (health informatics), na tiba
inayolengwa kulingana na sifa za mgonjwa (stratified medicine).
Unadhani
teknolojia kama hii inaweza kusaidia wagonjwa katika jamii yako?
Tuandikie maoni
yako na sambaza makala hii ili kuongeza uelewa kwa watu wengi zaidi.




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni