Jumamosi, 13 Aprili 2026 · Dar es Salaam, Tanzania
kijijichetumedia.com
Kijiji cha Habari Media
Kijiji cha Habari Media Simulizi za Mageuzi · SDGs · Tanzania
LEO
Fugakuku Business Solution yafunza wafugaji 2,000+ Tanzania — Soma simulizi yake hapa    •    Fugakuku Business Solution yafunza wafugaji 2,000+ Tanzania — Soma simulizi yake hapa    •   

Jumanne, 30 Desemba 2025

Kutoka kujitolea hadi mafanikio: Safari ya Misheck Lwenje na mapinduzi ya kilimo rahisi cha umwagiliaji

 MUHTASARI

Misheck Lwenje ni kijana wa Kitanzania aliyethibitisha kuwa kilimo ni ajira na biashara yenye tija. Kutoka kujitolea bila malipo hadi kujiajiri, Lwenje amewezesha zaidi ya wakulima 2,000 kupitia mbinu za kilimo biashara na umwagiliaji rahisi. Safari yake ilianza na mtaji wa Sh. 600,000 uliozaa shamba lenye thamani ya zaidi ya Sh. milioni 40, na leo anaongoza Kilimohalisi kama jukwaa la mafunzo, ajira na matumaini mapya kwa vijana na wakulima.



Ukiona posti zake kwenye mitandao ya kijamii akiwa ‘mchafumchafu’, huwezi kudhania kwamba Misheck Lwenje, ni kijana mwenye akili nyingi, ambaye amewafundisha wakulima zaidi ya 2,000 mbinu za kilimo biashara kwa umwagiliaji rahisi.

Lwenje mhitimu wa Chuo cha Kilimo Sokoine (SUA) mwaka 2015, ambaye yuko nyuma ya Kilimohalisi, hakuhitimu na kuanza kufundisha wakulima, bali kujitolea kwake, uvumilivu na nidhamu ya matumizi ya kila shilingi anayoipata, vimemfikisha alipo sasa.

Akiwa na Sh. 600,000 aliamua kununua shamba ambalo kimsingi ndio ofisi yake inayomwingizia kipato; na tayari limeongezeka thamani hadi zaidi ya Sh. milioni 40, ndani ya miaka minne.

Anafundisha matumizi ya kila kipande cha ardhi kwa kilimo cha biashara, kilimo bila kemikali, mbinu rahisi za umwagiliaji na umuhimu wa kupanda mimea ya kudhibiti wadudu waharibifu.

“Nilipomaliza haikuwa rahisi kupata ajira; kwa hiyo nikawa nimeomba kujitolea kampuni moja iko Iringa inayohudumia wananchi. Nikafanya kazi kama miezi sita nikawa silipwi, lakini nikawa napata maarifa na ‘connection.’

Anasema kujitolea kwake hakukuwa bure kwani miezi sita baadaye alikutana na watu wengi pamoja na taasisi mbalimbali, akiwamo mwajiri wake wa kwanza, kampuni ya kimataifa inayojishughulisha na kilimo kutoka Kenya.

Anasema mwishoni mwa mwaka 2016, kampuni hiyo ilisitisha kazi nchini na kulazimika kurejea Dar es Salaam kuendelea kujitafuta.



“Nikiwa nyumbani Dar es Salaam, alikuja rafiki yangu kwenye usaili, akashukia kwetu na ikalazimu asubuhi nimsindikize, tulipofika kwenye lile shirika (la Norway), jamaa aliyetupokea akasema basi ingieni wote (kwenye usaili)…maswali waliyouliza mimi nilikuwa nina uzoefu nayo kwa hiyo nikajibu vizuri sana, akasema atatuchukua wote kwa hiyo nikapata kazi.

“Tulikuwa tunawafundisha watoto yatima namna ya kujiajiri kupitia kilimo na tulikuwa tunafanya hivyo kuwaandaa kujitegemea.

“Baadaye wakaniambia niwafundishe wanawake kwenye Vikoba, kukawa na mkutano wa vikundi vya vikoba kutoka mikoa mbalimbali Tanzania. Hapa nikaendelea kuongeza maarifa na kujifunza zaidi,” anasema.

Lwenje anasema baada ya mkutano wa VIKOBA, viongozi waliomba mafunzo kwenye mikoa yao na ndipo yeye akapangiwa kwenda kufundisha wilayani Chunya, mkoa wa Mbeya.

“Tulikuwa tunawafundisha kufunga mfumo rahisi wa umwagiliaji…nilifanyakazi Mbeya, Songwe, Manyara na kisha Hai-Kilimanjaro hadi mwaka 2021 mkataba ulipoisha nikakataa kuendelea kuajiriwa,” anasema Lwenje.

Lwenje ambaye amejikita kwenye kilimo cha mboga, anasema kazi hiyo alianza kuifanya kwa kuzalisha miche na kuwafungia wakulima mfumo rahisi wa umwagiliaji.

“Unaona hii kazi ninayoifanya nilianza kuifanya bure, nilikuwa nazalisha miche, nawapa watu bure. Hata mfumo wa umwagiliaji nilikuwa nawapa watu bure. Nilitafuta site ambazo watu wengi wakipita wanaweza kuona…mtu akitaka kufanya kitu namwambia nenda kaangalie sehemu fulani, ukipenda uje tufanye kazi; nilianza kufanya bure, nikaanza kupata pesa baada ya watu kupenda.

“Nilitengeneza wakulima wa mfano na baadaye nikaanza kupata fedha. Nilianza kazi hii nikiwa na vijana wawili, lakini hivi sasa nina timu ya watu zaidi ya 20 ambao ninafanya nao,” anafafanua.

Mbali ya kufundisha wakulima, Lwenje anasema Kilimohalisi ni kiwanda cha kupika wataalamu wa kubobea kwenye kazi, wanaoweza kuajiriwa na kampuni yoyote.

“Mafanikio makubwa niliyopata ni kutengeneza watu ambao wanaweza kuajiriwa na watu wengine kutokana na kwamba wana uzoefu,” anafafanua.

FURSA KWENYE KILIMO

Anasema watu wanapaswa kufahamu kuwa mabadiliko ya tabia nchi yamepunguza uzalishaji wa chakula duniani, ilihali kuna ongezeko kubwa la watu wanaohitaji chakula kila siku.

“Nawaambia vijana kwamba kilimo ni fursa, hata kama atachelewa kuiona hela, lakini ataipata; cha kwanza kwenye kilimo kila mtu anahitaji chakula.

“Chakula ni sehemu nyeti sana duniani, ukiangalia hata magonjwa mengi tunayoyapata yasiyoambukiza asilimia kubwa yanasababishwa na chakula, tunakula vyakula ambavyo hatujui vimetoka wapi na amepiga dawa lini, hii ni changamoto kubwa.

“Fursa kwetu ni kubwa sana kwa sababu tunaweza kuzalisha chakula salama na tukaenda kuuza nje…hii ni fursa kwa vijana na kwenye soko la ndani fursa ni kubwa sana,” anafafanua Lwenje.

Anasema ili kufanikiwa kwenye kilimo, ni muhimu kuzalisha chakula kizuri kisicho na kemikali kwa kuzingatia muda wa kupiga dawa na kuvuna, ili kuwahakikishia walaji usalama wa afya.

Hata hivyo, anashauri ni muhimu kuwa na bustani ya mboga nyumbani ili kila familia ijipatie chakula salama.



ALIKOANZIA

Anasema safari ya Kilimohalisi ilianza mwaka 2019 alipopata Sh. 600,000 akanunua shamba ambalo limekuwa ofisi yake.

“Ni juzi tu kuna mtu amenifuata anataka kulinunua kwa Sh. milioni 40 nikakataa…lakini kama mwaka 2019 ningeamua kununua simu mpya nzuri au gari, nisingekuwa nayo na wala nisingekuwa na shamba. Ninachotaka kusema ni kwamba vijana tuwe na vipaumbele na sio kufanya vitu kwa kujionesha au kufuata mkumbo,” anasema.

Anasema badala ya kulalamika kukosa ajira, ni muhimu vijana wakafanya kazi kwa kujitolea kwenye mashirika au kampuni, ili kupata uzoefu na maarifa zaidi.

Anasema tangu alipojiajiri mwaka 2021, amefanikiwa kufundisha zaidi ya wakulima 2,000 wakiwamo aliowapa huduma bila malipo.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni