Mbinu hizi ni kwa wale ambao wanapenda bustani, lakini
hawana chanzo kizuri cha maji au pengine gharama za kulipia maji kwa ajili ya
bustani ya maua, ni kubwa.
Kama uko katika hali niliyoieleza hapo juu, soma makala
haya mpaka mwisho.
Mosi, ni vyema ukafahamu kwamba ipo mimea ambayo
inatumia maji kidogo na inahimili jua au hali ya ukame. Yapo yanayoweza
kuchanua mwaka mzima na pia yapo yasiyochanua. Ni muhimu kufahamu aina unayotaka.
Baadhi ya maua haya ni jesus, lavenda, kitenge,
fuhsia, alstromeria, kalanchoe, mandevile, jasmine, hibiscus, american palm (na
aina nyingine za palm), na nyasi aina ya buffalo (zile zenye majani mapana
kidogo).
Aina hizi pamoja na mengineyo, yanaweza kumwagiliwa
mara moja kwa wiki, yana sifa kubwa ya pekee ambayo ni kutodhuriwa kirahisi na
wadudu, hayavamiwi na mchwa na yanatumia maji, mbolea na virutubisho vingine
kwa kiasi kidogo sana.
Baada ya kuchagua aina ya maua, tengeneza ratiba ya
kuyamwagilia. Hapa inashauriwa ufunge mfumo wa umwagiliaji wa matone, ili maji kidogo
uliyonayo yafike kwenye mmea wako bila kupotea.
Mfumo huu utakupunguza matumizi ya maji kwa kiasi
kikubwa, huku ukiendelea kufurahia mandhari ya kupendeza.
DONDOO MUHIMU
· Chagua
mimea inayostahimili ukame hasa miti, maua ya asili na nyasi za mapambo na
kuipanda kulingana namna eneo lako lilivyo.
· Zingatia
ukubwa na umri wa mmea, mimea yenye mizizi mirefu huwa na uwezo mkubwa wa
kustahimili ukame kuliko miche michanga.
· Fanya
usimamizi makini wa udongo, kwa kuongeza samadi, ili kuongeza uwezo wa
kuhifadhi unyevu na kusaidia mifereji ya maji na pia unaweza kutandaza majani
makavu kuzunguka mmea, ili kutunza unyevu.
· Ongeza
sehemu za kupita, weka mawe au kokoto katika baadhi ya maeneo, ili kupunguza
mimea na hivyo kupunguza matumizi ya maji. Mawe huongeza uzuri wa asili.
· Unaweza
kupanda lavenda, jesus, jasmini, rosemary na minti, ambayo yanahitaji matunzo
kidogo na inastahimili ukame.
·
Mwagilia mapema asubuhi au jioni jua
likiwa limezama, ili kupunguza upotevu wa maji.
·
Ondoa magugu mara kwa mara kwa kuwa
kuwapo kwa mimea vamizi bustanini kwako, kunasababisha magugu na maua yako kugombea
maji pamoja na virutubisho vingine.
·
Kwenye mawe, tumia yenye ukubwa
tofauti ili kuongeza mvuto asilia.
Aidha, pamoja na kwamba maua haya
yanahimili jua, ukiyaweka kivulini yanafanya vizuri zaidi, kwa hiyo nakushauri
pamoja na uwezo wake mkubwa wa kutumia maji kidogo, unaweza kupanda miti
kadhaa, ili kutengeneza kivuli kwa ajili ya maua yako.



Hakuna maoni:
Chapisha Maoni